Maandamano hayo yaliyofanyika kwa mnasaba wa kutimia mwaka mmoja tangu Morocco ianzishe uhusiano wa kawaida na utawala vamizi wa Israel yaliandaliwa na Jumuiya ya Morocco ya Kuunga Mkono Palestina na Kupinga Kuwa na Uhusiano na Israel yameshirikisha matabaka mbalimbali ya jamii.
Waandamanaji wenye hasira walichoma moto bendera za Israel na kupiga nara za kupinga kuanzishwa uhusiano na utawala huo ghasibu. Aidha waandamanaji hao, wameitaka serikali ya Morocco kufutulia mbali mkataba iliotiliana saini na Israel wa kuwa na mahusiano baina yao. Vikosi vya usalama vya Morocco vilivamia maandamano hayo na kuwatawanya waandamanaji.
Ikumbukwe kuwa, nchi nne za Kiarabu za Imarati (UAE), Bahrain, Morocco na Sudan mwaka uliopita wa 2020 zilisaini hati za makubaliano ya kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala haramu wa Kizayuni, hatua ambayo imepingwa na kulaaniwa vikali katika nchi za Kiarabu na Kiislamu.
Sudan, Morocco na Bahrain zimeendelea kushuhudia maandamano kila leo ya wananchi ya kulaani na kupinga hatua ya nchi zao ya kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala haramu wa Israel. Wananchi waliowengi katika nchi hizo wanasema kuwa, hatua hiyo ni khiyana na usaliti mkubwa kwa wananchi wa Palestina wanaofanyiwa unyama wa kila aina na utawala wa Israel kila uchao.