Muhammad Baqer Qalibaf, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema katika ujumbe wake huo kwamba, mwezi mtukufu wa Ramadhani ni fursa ya kumuomba Mwenyezi Mungu atuepushie janga hili la vitusi vya COVID-19 na fursa nzuri ya kuimarisha umoja na mshikamano wa Umma wa Kiislamu.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema pia katika ujumbe wake huo kwamba: "Ninaamini kwa moyo wa dhati kabisa kwamba, kuimarisha umoja na mshikamano baina ya nchi za Waislamu katika mazingira haya ya sasa maalum na ya dunia nzima, kutapelekea kupatikana uthabiti, usalama, utulivu wa kudumu na afya na uzima katika Ulimwengu wa Kiislamu."
Spika Qalibaf ametumia fursa hiyo pia katika ujumbe wakke huo kusisitiza kwamba, Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran sambamba na kusisitiza udharura na umuhimu wa diplomasia ya kibunge katika ulimwengu wa leo, linakaribisha kwa mikono miwili suala la kuimarishwa ushirikiano na mahusiano mazuri baina ya mabunge ya nchi za Kiislamu kwa ajili ya kuleta maelewano, umoja na mshikamano ili kwa njia hiyo iwezekane kuipatia ufumbuzi migogoro mbalimbali katika Umma wa Kiislamu.