Akizungumza katika kikao na waandishi habari leo Jumatano mjini Tehran, Ali Reza Rashidian amesema Iran ilikuwa imekamilisha mipango yote ya kuwatuma Mahujaji Saudia lakini kwa masikikitiko Hija ya mwaka huu imefutwa.
Saudia ilitangaza Jumatatu kuwa ni watu wachache sana watakaoruhusiwa kuhiji mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia imesema kuwa, Hija ya mwaka huu itashirikisha idadi ndogo ya mahujaji ambao ni raia wa Saudia na raia wa kigeni ambao ni wakazi wa nchi hiyo. Hatua hiyo ya kuwazuia mahujaji kutoka nje ya Saudia imechukuliwa kutokana na kuendelea maambukizi ya ogonjwa wa COVID-19 ambao haujapatiwa chanjo wala dawa.
Mwezi Machi mwaka huu pia Saudi Arabia ilisimamisha ibada ya Umrah kwa Waislamu kutokana na maambukizi ya virusi vya corona. Wakati huo Wizara ya Hija na Umra iliwataka Waislamu kote duniani kusubiri kabla ya kuchukua hatua yoyote ya kujitayarisha kwa ajili ya ibada ya Hija.
Iran ilikuwa inatarajiwa kutuma watu zaidi ya 85,000 kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu.