IQNA

Kiongozi Muadhamu na Masuala ya Kimataifa

Kiongozi Muadhamu abainisha sababu za hali maalumu inayotawala duniani

19:08 - May 25, 2022
Habari ID: 3475295
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amebainisha sababu za hali maalumu duniani sasa na kusema kusema katika hali ya sasa ya dunia, uendeshaji mambo umekuwa mgumu kwa nchi zote.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo mjini Tehran katika mkutano na wabunge wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge).

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria ukubwa, idadi ya watu, jiografia, historia na hali tofauti za hali ya hewa zilizopo Iran na akasema: uendeshaji nchi kulingana na nafasi iliyonayo nchi yetu azizi ni kazi muhimu; na kwa kuzingatia mazingira maalumu ya dunia hivi sasa, ni mgumu na tata.

Ayatullah Khamenei ameongezea kwa kusema: bila ya shaka katika hali ya sasa ya dunia, uendeshaji mambo umekuwa mgumu kwa nchi zote.

Katika kubainisha sababu za hali maalumu inayotawala duniani, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema: ushindani wa kihasama baina ya madola, vitisho yanavyotoleana madola ya atomiki, harakati na vitisho vinavyoongezeka vya kijeshi, vita vinavyojiri eneo la jirani na Ulaya linalojulikana kama moja ya maeneo yenye hatari kubwa zaidi ya kutokea vita duniani, kusambaa kwa maradhi kwa kiwango nadra kuwahi kushuhudiwa na hali hatarishi ya uhaba wa chakula duniani kote, yote hayo ni mambo ambayo yameyafanya mazingira ya dunia wakati huu yawe ya kipekee; na katika hali kama hii uendeshaji nchi umekuwa mgumu zaidi na tata zaidi.

Ayatullah Khamenei amefafanua zaidi kwa kusema: mbali na mazingira yanayotawala katika nchi zote, Iran, -ambayo kwa sababu ya kuleta mfano mpya wa kuigwa, wa mfumo wa utawala wa kidini unaotokana na ridhaa ya wananchi, na ambao umevuruga nidhamu iliyoratibiwa na mfumo wa ubeberu- inakabiliana na changamoto za kudumu za madola ya dunia katika sura tofauti.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imesimama imara kukabiliana na kila aina ya uadui na uhasama na inaendelea kupiga hatua za maendeleo na mafanikio na akaongeza kwamba: Wabunge, Serikali, Idara ya mahakama na wahusika wa vyombo vyengine vyote inapasa waelewe ukubwa na umuhimu wa nyadhifa za uongozi walizonazo na wazidi kujichunga nafsi zao kulingana na nyadhifa hizo.

Kwingineko katika hotuba yake, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa kuendelea kubaki kuwa mwanamapinduzi ni muhimu zaidi kuliko kuwa tu mwanamapinduzi.

Katika mkutano huo na Spika pamoja na wabunge, Ayatullah Khamenei amesema, kukombolewa mji wa Khoramshahr ni nembo ya mabadiliko ya mlingano wa ladha tamu badala ya chungu na kuthibiti uokovu wa kitaifa; na akaashiria baadhi ya sababu za kubadilika mlingano huo kwa kusema: kanuni ya kuwezesha kuvuka mazingira magumu, tata na ya machungu na kufikia ushindi na mafanikio ni kufanya mambo kijihadi, kwa azma thabiti, kwa ubunifu wa matendo, kujitolea mhanga, kuwa na uono wa mbali na muhimu zaidi ya yote hayo, kuwa na ikhlasi na kumtegemea Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Amelitaja bunge kuwa ni moja ya nguzo kuu za uendeshaji nchi na akasisitiza kwa kusema: "kuwa na utambuzi sahihi wa uwezo uliopo na udhaifu uliopo ni moja ya masuala muhimu sana, kwa sababu adui ameelekeza zaidi matumaini kwenye kasoro na makosa yetu kuliko uwezo wake mwenyewe alionao."

4059599

captcha