Kwa mujibu wa taarifa, watu watatu wamefariki katika mji wa Bangalore nchini India baada ya maafisa wa polisi kuwafyatulia risasi waandamanji waliokuwa wakiandamana dhidi ya chapisho la lenye kumvunjia heshima Mtume SAW katika mtandao wa facebook.
Makundi ya watu yalikusanyika nje ya nyumba ya mwanasiasa mmoja ambaye ndugu yake alituhumiwa kuchapisha chapisho lenye kumvunjia heshima Mtume SAW.
Kamishna wa mji huo Kamal Pant alisema mwanasiasa huyo, Naveen Kumar,amekamatwa. Pant pia amesema kwamba takriban maafisa 60 wa polisi akiwemo afisa mmoja mkuu walijeruhiwa katika ghasia hizo siku ya Jumanne usiku. Masharti ya kutotoka nje yaliwekwa katika wilaya mbili za eneo hilo, alisema.Vifo hivyo vilithibitishwa na waziri wa jimbo la Karnataka ambapo Bangalore ndio mji mkuu.
Ghasia hizo zilianza baada ya waandamanaji kupiga kambi nje ya nyumba hiyo ya mwanasiasa mbali na kituo kimoja cha polisi baada ya kuliona chapisho hilo, ambalo vyombo vya habari vinasema limefutwa.
Wanazuoni na wanasiasa Waislamu wametoa wito kwa watu wajiepushe na ghasia.
Tangu ilipoingia madarakani serikali ya Narendra Modi nchini India, kumeshtadi mashambulizi ya maafisa usalama na Wahindu wenye misimamo mikali dhidi ya Waislamu wakiwemo wa eneo la Kashmir.
Chama tawala India cha Baratiya Janata (BJP) cha Narendra Modi ambacho kinaendesha siasa za mielekeo na misimamo ya kitaifa ya uchupaji mipaka katika miongo ya karibuni kimeonesha rekodi hasi sana ya namna inayoamiliana na Waislamu.